Mbegu za ufuta zina faida nyingi kiafya na kiuchumi. Hata hivyo, mavuno ni machache barani Afrika kwa mbinu duni za upanzi kama vile kutawanya mbegu. Kupanda ufuta katika safu pamoja na kupunguza miche kunaweza kusaidia kupanua mavuno.
Kupanda kwa kutawanya husababisha ukuaji wa mimea iliyosongamana sana kwa hivyo, mimea hukua vibaya. Pia kunafanya shughuli za shamba kama vile kupalilia kuwa ngumu. Kwa kupanda ufuta katika safu na kupunguza miche, mimea hupata nafasi ya kutosha, na hivyo hukua vyema na kutoa mavuno mengi. Ili kuwa na shamba nzuri la ufuta, tumia mbegu bora ambazo zinaota vizuri. Panda mbegu wakati ambapo mimea inatarajiwa kuvunwa, wakati usio na mvua. Ufuta hukomaa katika miezi 3 baada ya kupanda.
Njia ya kupanda
Kabla ya kupanda, lima na ulainishe udongo kwa sababu mbegu za ufuta ni ndogo na huota vizuri kwenye udongo laini. Panda safu za ufuta kwenye shamba lenye matuta ukiacha nafasi ya umbali wa cm 80 kati ya safu hizo, au kwenye shamba tambarare kwa muachano wa 60 cm. Kufanya huku husaidia mimea kukua vizuri na hufanya upaliliaji wa magugu, na uvunaji kuwa rahisi. Unapopanda, acha umbali wa cm 20 kati ya mashimo ya kupandia.
Ili kuepusha kuweka mbegu nyingi katika shimo moja, changanya kipimo kimoja cha mbegu za ufuta na vipimo viwili vya mchanga uliyokauka au wishwa. Unapotumia kifaa cha kupandia, ni bora uchanganye mbegu na wishwa. Wakati wa kupanda, chimba mashimo ya kina kifupi na kuweka mbegu, kisha uzifunike kwa udongo kidogo.
Baada ya wiki 1, unaweza kupunguza miche na kujaza pengo kwenye mashimo yasiyo na miche. Vile vile unaweza kufanya huku pamoja na kupalilia kwa kwanza katika wiki 3. Unapopunguza miche, acha mimea 2 yenye nguvu kwa kila shimo. Kupanda kwenye safu na kupunguza miche hurahisisha kupalilia, kuvuna na kufunda mabunda.